Tuesday, November 8, 2016

HADITHI: Msamaha Wa Mama

 
Na Saed Bin Salim
Mwanzo
Kumbukumbu…..
Mama! Kila siku nakuuliza kuhusu baba yangu yuko wapi hunijibu na kunambia utanambia! utanambia! utanambia, nina miaka tisa sasa hivi simjui baba yangu. kwa nini lakini mama! kuna kitu gani hasa kikubwa kinakufanya usinambie ukweli kuhusu baba, naomba uniambie tafadhali mama. nakuomba usinifiche, shuleni kila siku tunasoma “mficha maradhi kifo umuumbua” na bora aibu kuliko fedheha, au unahisi mimi nakuwa katika hali nzuri ninapowaona marafiki zangu wapo na wazazi wao wote wawili?
Hiyo ilikuwa kumbu kumbu ya maneno nliyoyakumbuka kipindi nimelala chali katika kitanda ambacho huwa analala mama yangu na mimi kulala chini kutokana na hali duni ya maisha tuliyonayo.
swali hilo lilinifanya nikumbuke mengi sana yaliyotokea nyuma kipindi nna miaka tisa, nkamkumbuka sana mama yangu ambae wakati huo alikuwa ameenda kumtembelea bibi shamba.
Swali nlilomuuliza mama miaka 11 nyuma usiku mmoja wa saa mbili tuliokuwa tumekaa chini chumbani baada ya kumaliza shuguli zote za hapa na pale, lilimfanya mamaangu kipenzi aanze kuonesha dalili ya machozi machoni mwake. alitingisha kichwa. nlipomuangalia nkajua anaashiria kunisikitikia sana. aliinuka chini tulipokuwa tumekaa akashusha pazia ambayo huwa tunaitenganisha kati kwa kati chumbani, akapita upande wa pili ambao kulikuwa na kitanda chake, alilala huku machozi yakianza kumlenga akifikiria swali nlilomuuliza.
Nlimuita mara kadhaa lakini hakuitika, nkajua nimemkosea sana mama angu nkamuambia anisamehe kama nimemkosea, kwani sikuitaji hata siku moja akose furaha kwa ajili yangu.
nliinuka kwenye kigoda nlichokuwa nimekaa na kuingia kwenye neti iliyokuwa imeegeshwa kwenye mkeka nliokuwa naulalia chini siku zote nkalala.
nlikuwa mtoto lakini akili zangu zilikuwa za kiutu uzima, nlizima kibatali na kulala huku nkiwa na mawazo ya kuhisi kumkosea mama yangu kwa kumuuliza kuhusu baba japo ni wajabu wangu kuuliza swali hilo kwake, kwa sababu sikuwai kumuona tokea kuzaliwa kwangu. Tokea nlipojitambua naangaza macho na kumuona mama akiangaika peke yake juu yangu bila kujua baba yuko wapi. Kitu kilichokuwa kinanipa wakati mgumu hata nlipokuwa shule..
Wakati tayari nimelala na kuweka neti vizuri nkiichomeka chini ya mkeka.  kwa mbali nlisikia kilio cha chini kwa chini nkageuza uso wangu ili kusikiliza vizuri kilio kinatokea wapi, bado sikufanikiwa licha ya kugeuza uso ikabidi niinue shingo yangu nkitega masikio yote mawili. ndo nligundua anaelia chini kwa chini ni mama yangu. Nlitamani nifunue pazia nimfate na kumuuliza kitu gani kinamliza au ni kwa sababu ya swali langu nlilomuuliza, lakini nkashindwa kwa sababu sikujua yuko katika hali gani, nliofia kufunua pazia nkiogopa kumkuta yuko uchi au katika mavazi ya kuonesha maungo yake.
Ilinibidi Nimuite na nlimuita zaidi ya mara tatu bila kuitika, hasira zilinishika nkageuka upande wa pili nkajikunja huku nkivuta shuka langu la kujifunika, nkajifunika na kuweka vidole masikion ili nsisikie kilio cha mama yangu kipenzi ambae nlimfanya wa pili kwa umuhimu baada ya Mungu alie juu.
namshukuru Mungu kutokana na uchovu nliokuwa nao wa shule pamoja shambani hazikupita dk tatu nlipitiwa na usingizi ulionipeleka mpaka saa kumi na mbili na dk 5 asubuhi nkaamka na kujiandaa kwa ajili ya kuwahi namba shuleni. Nlinawa uso nkavaa nguo na kupaka mafuta mgando ambayo nlikuwa nahakikisha yamerundikana usoni.
Nlipomaliza kuvaa kila kitu nlichukua mkoba wangu uliokuwa tayari umechanika chanika baadhi ya sehemu nkauweka mkono upande kisha nkamuita mama ili anipe chochote kitu kama kipo cha kutumia shuleni.
“Mama naenda shule. nlimuambia mama baada ya kumuita na kuitika, ikiwa kama style ya kumsikilizia atasemaje kama mzazi.
“Ok mwanangu nakutakia masomo mema, kuna shiling mia hapo juu ya mfuniko wa ndoo, ichukue ikifika saa nne utanunua hata bagia ule saa nane ukirudi utakuta chakula tayari. Hali yetu ni masikini mwanangu usije kuona wivu kwa kuwaona wenzio huko shule wanakula vitu vya bei, ni kwa sababu wazee wao wana pesa.
Hayo ndo yalikuwa maneno ya mama akiongea kwa hali ya usingizi.
nliitikia “Haya” nkaangalia juu ya mfuniko na kukuta shiling mia tu, nliichukua na kuiweka mfukon nkamuaga mama mara ya mwisho, nlifungua na kufunga mlango nkatembea haraka haraka kuwahi Namba na kwaride la shule lililokuwa linaanza saa moja na nusu.
” Ah mtoto wa mama huyooooooo!!!
Kama kawaida ya tabia ya watoto wa shule ilivyo, kipindi natembea nlikutana na kundi la wanafunzi waliokuwa wanasoma darasa la nne wakati mi niko la tatu.
ilikuwa si mara yao ya kwanza kunambia maneno hayo kila waliponiona, ni maneno ambayo nlishayazoea kutoka kwao kutokana kuniona kila siku nkiishi na mama yangu bila baba, kibaya zaid nkilala nae chumba kimoja kila siku.
Ni maneno ambayo yalikuwa yakinikera sana kiukweli moyoni japo nlikuwa mtoto, na hasira zote nlizokuwa natoka nazo hapo zilikuwa zikiishia kwa mama  kumuuliza swali lililokuwa ni gumu sana kulijibu siku zote nlizokuwa nkimuuliza.
Waliendelea kuniteta kwa kusema maneno yaliyokuwa yakizidi kuniumiza moyoni mwangu kwakweli.
“Mtoto wa mama mbona hutujibu wewe?. ” Muacheni bhana amezoea kudeka kwa mama yake huyoo……
Ila sikujali maneno yao kwa sababu nlishayazoea na huwa yanantia hasira sana, na tayari nlikuwa nawahi shuleni sikuitaji hata siku moja kupata adhabu toka kwa walimu au viranja kwa sababu ya kuchelewa mstarini au kwa ajili ya utovu wa nidhamu.
Nlifanikiwa kuwahi mstarini nyimbo ya taifa ilianza kuimbwa, baadae tukaesabu namba na kuingia darasani. Upo muda ambao nlipokuwa darasan nliishia kushika tama kutokana na mawazo mazito ya kuitaji kujua aliko baba yangu, na kujiuliza kwa nini mama nkimuuliza swali kuhusu baba huwa anakasirika, na bora angekuwa anakasirika alafu ananijibu lakini huchukua maamuzi ya kutoka sehemu tunayokuwa tumekaa kabisa machozi yakiwa nje nje…
Saa nane ilipofika  nliwahi nyumbani haraka kutokana na njaa iliyokuwa imenikamata, Namshukuru Mungu siku hiyo nlikuta viazi vinne kwenye sufuria baada ya kufika. kwani siku nyingine huwa sikuti kitu kabisa. Nlinawa na kuanza kula pembeni nkiwa na kombe la maji, nlipomaliza nliingia shambani kumuangalia mama.
nlifanikiwa kumuona akiwa anapariria viazi vitamu vilivyokuwa vimezungukwa na magugu, nlitingisha kichwa kwa kumuonea huruma mama, Jua la saa nane lote lilikuwa likimuingia mwilini. nlimfata na kumuamkia
“Mama shkamoo
Aligeuka akaniangalia huku akiitikia shikamoo yangu.
“Marahabaa mwanangu umerudi baba.”
“Ndiyo mama nimerudi.”
“Mmesoma shule.”
“Ndiyo tumesoma kiswaili na haiba ya michezo.”
“Ok mwanangu umepata vizuri?
” ndiyo nimepata mama.”
“Haya mwanangu soma uje unisaidie mama yako si unaona nnavyoangaika hapa.”
Sikumjibu swali hilo pembeni kulikuwa na dumu la maji pamoja na kikombe, niliyafuata nikamimina na kunywa, nilipomaliza aliniuliza.
“Ushakula?
“Ndiyo nimekula. Nilimjibu huku nikimezea maji ya mwisho.
“haya itabidi ujiandae sasa uje hapa unisaidie.
Nlijisikia vibaya baada ya kunambia hivyo, nilijikuta namuambia nikiwa natamani kulia
“Bhana mamaa!!,Ah, nimechoka mimi!
“Mwanangu najua umechoka ila chakula chetu ndiyo hiki hiki tutafanyaje? hata mimi nimechoka lakini najikaza mwanangu.
“Aah! Sawa.
nIlitoka pale nIkiwa nimevimbisha uso wangu, niliingia ndani na kubadilisha nguo nikarudi shambani kwa ajili ya kumsaidia mama.
Jua la mchana lote lilituishia mwilini, mpaka saa kumi na mbili ndiyo tulitoka shambani tukiwa na viazi vitano kwa ajili ya kupika usiku.
Nilipofika nje ya nyumba nilitua mzigo mdogo wa kuni niliokuwa nao begani, nikachukua vidumu viwili vya maji kwa ajili ya kwenda kuchukua maji kisimani.
Uchovu mkubwa nilikuwa nao wakati huo ila nilijua kuchota maji ni wajibu wangu, na ndani kulikuwa hakuna maji hata kidogo na mama anatakiwa kuoga. Ilinilazimu kwakweli nisingekubali kumuona mama anabeba vidumu kwenda kuchota maji wakati mimi nipo. hata niwe nimechokaje.
Nilipofika bombani nilishangaa kuwaona watoto ambao nao wana kawaida ya kunitania. Nilitamani kurudi nyuma lakini tayari walishaniona, Nilisogea hadi kisimani nIkiwa nimekunja uso wangu, walinangalia bila kunimaliza mimi nikiwa nimeshikilia kifaa cha kuingiza kisimani kuteka maji na kuingiza kwenye vidumu nlivyokuwa navyo.
Ukimya ulitanda muda niliofika na kuanza kuteka maji, nilijaza vidumu vyangu vyote viwili, vilipojaa nikabeba kwa ajili ya kuondoka.
“Hahahaaaaaa Mtoto wa mama huyooo lione Sura nyeusi kama usiku. Alisema mtoto mmoja kati yao aliyeitwa mudy nilipokuwa tayari nimewapa mgongo, ni kama walikuwa wananiteta mioyoni mwao.
” Muacheni huyo amezoea kunyonya maziwa ya mama, jitu zima bado linalala na mama yake iloooooooo lione.
“Kwani hana baba yule? Aliuliza mmoja wao.
“mama yake alikuwa malaya huyo anatembea na wanaume tofauti akapigwa mimba ndiyo akapatikana huyu mjinga, muone vile.”
Ni maneno ambayo yaliniuma sana walipoyaongea baada ya kuwapa mgongo, niliweka vidumu chini mbele yangu nikayaona mawe matatu, niliyaokota na kuwarushia moja baada ya lengine kwa hasira nilizokuwa nazo, Moja ya watoto hao waliokuwa watano jiwe lilimpata na kumjeruhi vikali karibu na jicho lake la kulia, wote waliingiwa na mshangao wa “Haaaaa” huku huyo aliejeruiliwa akiinama chini  na kuanza kulia.
Nilipoona hivyo nilikimbia na kuviacha vidumu, walimuacha mwenzao wakanifukuza lakini hawakunipata kutokana na wepesi wa mwili wangu niliokuwa nao pamoja na mbio.
Nlifika nyumbani na kuingia ndani moja kwa moja, mama alikuwa jikoni akashangaa kuona natoka huko nkiwa mbio. waliokuwa wananifukuza walifika na kumwambia mama anitoe ndani huku wakiwa wanahema.
“Mama Seid mtoe mwanao ndani haraka na sisi tumfanyie kile alichomfanyia mwenzetu.
“Kuna nini kwani jamani nyie watoto? Mama aliuliza kwa mshangao.
“Unajifanya hujui?, mwanao si ndiyo unavyomfundisha hivyo awapige watu mawe.
“Mnasemaje nyie watoto! (mama aliongea akionekana kuchukia kwa alichoambiwa)  yaani hamna adabu kiasi hicho kumbe.
“Adabu tayari tulishawapatia wazazi wetu tukupe adabu wewe nani kwani? mtoe mwanao ndani tumpige jiwe kama alivyomfanyia mwenzetu.
Watoto waliongea kwa jeuri, ni kama walikuwa wanamfokea mama yangu wakati hawampati hata kwa robo kiumri.
Niliumia sana kusikia wanavyomjibu mama, nikatoka ndani na panga kwa hasira, waliponiona walikimbia na mimi nikawafuata kwa nyuma, sikuweza kuwapata lakini kama ningewapata nadhani ningeua kutokana na kile ambacho tayari kilikuwa moyoni mwangu.
Nilirudi na kuliweka panga chini huku nikiwa nimevimbisha mdomo, Mama alishika kiuno na kuachia mguno wa “hhhmmm” akishusha pumzi zake.
“Seid umeanza utundu na wewe wa kupigana na wenzio si ndio. Nilishindwa kujibu swali lake, akaniuliza tena akionekana kukasirika na kile nilichokifanya.
“Mama kila siku nakuuliza kuhusu baba hunijibu, kila nikikuuliza hunijibu, kila nikikuuliza hutaki kunijibu kwa nini lakini mama? Mimi siyo mtoto kama unavyofikiria, sawa mimi ni mdogo nina miaka tisa tu lakini nina akili za kufikiria mbali, pia nina wajibu wa kuwaona wazazi wangu wote wawili, baba yuko wapi?
Nambie ukweli mama, kama alishafariki sema? haiwezeani mimi naenda bombani naambiwa mama yangu ulikuwa Ma, ma (nlishindwa kuongea hilo neno malaya, japo tayari nilishakasirika lakini ufahamu wa kujua aliyoko mbele yangu ni mama yangu mzazi uliniingia),
kiukweli niliongea kwa hasira sana mama akiwa amesimama na kuniangalia, alinambia nimalizie kile nilichokikatisha ndiyo nikamwambia:
“Naambiwa kuwa ulikuwa unawabadilisha wanaume kila siku ndiyo maana umenipata mimi na ulipata ujauzito bila kutegemea ndiyo maana hujui baba yangu yuko wapi, japo siamini hayo maneno kwa sababu wale walionambia ni wadogo hawakuwepo wakati huo lakini baba yangu yuko wapi?
Nijibu mama usiishie kulia tu kila nikikuuliza..
Machozi yalishaanza kunitoka, mama naye tayari alikuwa anabubujikwa na machozi kwa nilichomwambia.

Usikose sehemu ya pili ya mwendelezo wa simulizi hii .

TANZIA:Aliyewahi kuwa Waziri wa elimu awamu ya tatu, Joseph Mungai afariki dunia



Aliyewahi kuwa waziri wa Elimu Tanzania Joseph Mungai amefariki Dunia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu
Geofrey Mungai mtoto wa Marehemu amesema marehemu alipelekwa hospitali ya Taifa Muhimbili baada ya kuanza kutapika mfululizo na kudhaniwa kwamba alikuwa amekula kitu kibaya.

BUNGENI: Serikali Yaitaka sekta binafsi kuwekeza katika kinywaji aina ya Gongo ili kurasimisha kinywaji hicho



Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amezishauri kampuni zinazotengeneza vilevi kutengeneza pombe yenye ladha ya gongo, kwa kuwa  baadhi ya wateja wanavutiwa na ladha hiyo wana wanakipenda kinywaji hicho.

Mwijage ameyasema hayo leo bungeni mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Gimbi Masaba (Chadema) aliyehoji mpango wa serikali wa kuanzisha na kuhalalisha viwanda vya kutengeneza pombe aina ya gongo ili kuchochea uchumi wa nchi na kubainisha kuwa, gongo ikitengenezwa kiwandani itafuata ubora unaotakiwa kisheria.

“Moja ya kigezo muhimu cha kuanzisha kiwanda ni uwepo wa soko, kutokana na wananchi kupenda kinywaji hiki(gongo) nawashauri wadau wa sekta hii kuwasiliana na ofisi za Sido ambazo zinapatikana mikoa yote ili kupata muongozo juu ya uanzishaji wa viwanda bora na salama vya aina hii,” alisema Mwijage.

Amesema haiwezekani Serikali kuhalalisha gongo, ila inaishauri sekta binafsi kuanzisha viwanda vitakavyotumia malighafi zinazotengeneza kinywaji hicho kwa lengo la kuzalisha kinywaji kinachokidhi viwango vya usalama na ubora wa chakula.

Katika swali la nyongeza, Masaba amehoji kama serikali ipo tayari kufanya utafiti kujua faida zilizo kwenye gongo.

Mwijage amesema faida zinafahamika, lakini atawaelekeza wataalamu wake waendele maeneo yenye gongo na pombe nyingine za kienyeji ili kuzifanyia utafiti na zitengenezwe kwa kufuata ubora na viwango.

Kangi Lugola Adai Mkataba wa EPA Utatuletea USHOGA


Mbunge  wa Mwibara Kangi Lugola, ameupinga  kwa  nguvu  zake zote  mkataba  wa EPA kwa madai kwamba hauna manufaa yoyote kwa taifa letu na kwamba ndani ya mkataba huo kuna vishiria vya USHOGA
Lugola aimeitaka serikali isiusaini mkataba huo ili kulinda maumbile ya wanaume yanayotaka kuharibiwa kupitia mkataba huo.
Msikilize hapo chini alipokuwa akitoa mchango wake bungeni

Chadema watinga Mahakama Kuu kutaka Lema ashtakiwe


Chama Cha Demokrasia na Meendeleo (Chadema), jana kilifungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, wakipinga kitendo cha Jeshi la Polisi kumuweka rumande mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema kwa zaidi ya saa 175 bila kumpeleka Mahakamani.

Mwanasheria wa chama hicho, John Mallya jana aliwaambia waandishi wa habari katika viwanja vya mahakama hiyo kuwa wamefungua kesi hiyo kwakuwa sheria inaelekeza mtuhumiwa kutozidi saa 24 mahabusu bila kufikishwa mahakamani, hivyo kitendo cha kumshikilia Lema kwa zaidi ya muda huo ni kinyume cha sheria.

Katika kesi hiyo, chama hicho kimeiomba Mahakama kuwaamuru Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Mkuu wa Polisi wa Arusha na Mkuu wa kituo cha Arusha (Central) kumpeleka mahakamani mbunge huyo.

Mallya aliongeza kuwa anakamilisha mchakato wa kukusanya hati ya wito wa kuitwa mahakamani kwa vigogo wa Polisi pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili waweze kueleza ni kwanini wamekiuka masharti ya kisheria ya kutomshikilia mtu kwa zaidi ya saa 24 bila kumfikisha mahakamani.

“Tunataka hawa tuliowashtaki kumleta Lema mahakamani na dhamana yake ifanyiwe mchakato Mahakama Kuu na waiambie mahakama kwanini wasichukuliwe hatua za kisheria, pia tumeomba gharama zote za hii kesi zilipwe na Serikali,” Mallya aliwaambia waandishi wa habari.

Lema alikamatwa Jumatano iliyopita akiwa Bungeni mjini Dodoma na kusafirishwa hadi jijini Arusha kwa tuhuma za kutoa maneno ya kichochezi dhidi ya Rais John Magufuli.